ROBOTI XINGHZE1 ATEMBEA KILOMITA 134 KUWEKA REKODI MPYA

Roboti aliyepewa jina la Xinghze No. 1 aliyetengenezwa nchini China, amevunja rekodi ya Dunia ya 'Guinness World Records' kwa kutembea kilomita 134.03 ambazo ni sawa na maili 83.28 (83.28 miles).


Roboti huyo aliyetengenezwa na team iliyoongozwa na Profesa Li Qingdu kutoka College of Automation of Chongqing University of Posts and Telecommunications.

Roboti huyo aina ya Quadruped ametengenezwa kwa mashine moja ambayo inaongozwa na program ya kompyuta au sakiti moja ya umeme. Pia, roboti huyo ameundwa kwa miguu minne (Four legs) isiyo na magurudumu (wheels).

Mwongozo uliotolewa na Guinness World Records ni kwamba ili Roboti avunje rekodi ya Dunia kutembeanumbali mrefu, anatakiwa kuchajiwa mara moja au kutumia tanki moja la mafuta na pia anatakiwa atembee mfululizo kwa masaa takribani 54 na dakika 34 ili kuipiku rekodi inayoshikiliwa na jopo Chuo Kikuu cha Cornell Ranger Robot ambapo roboti wao alitembea umbali wa kilomita 65.18 sawa na maili 40.5, roboti Walker 1, alivunja rekodi hiyo jijini New York Marekani mwaka 2011.

Kwa mujibu wa Profesa Qingdu utafiti wa roboti huyo ulianza mwezi Novembea mwaka jana 2014 na alisema kuwa lengo la kutengeneza roboti huyo ni kuelewa ufanisi wa umeme, kuongeza umbali ambao roboti anaweza kutembea, ufanyaji wa kazi, uwezo wa kupingana na kani za nguvu na uwezo wa roboti kutimiza malengo katika hali ambazo zinaweza kuwa hatari kwa binadamu.



Chanzo: Guinness World Records


BIBI WA MIAKA 85 AKAMATWA KWA KUIBA HERENI

Bibi kizee mmoja mwenye umri wa miaka 85 raia wa Marekani na ambaye amekuwa akiiba vito vya thamani kwa zaidi ya miaka 60 amehukumiwa tena kwa kosa la wizi.

Doris Payne, anatuhumiwa kwa wizi wa herini ya thamani ya dola 690, kutoka katika duka moja la uuzaji wa vitu vya thamani la Saks katika kiunga kimoja mjini Atlanta-Marekani.

Wakili wake anatafuta namna ataachiwa huru kwa sababu ya kudorora kwa afya yake.

Payne, ambaye maisha yake ya wizi yaliwekwa katika filamu mwaka 2013, amewahi kufungwa jela mara kadhaa kwa makosa mengi tu ya wizi na uhalifu.

Wakuu nchini Marekani wanasema kuwa, ametumia majina 22 ya bandia tangu alipoiba almasi kwa mara ya kwanza akiwa na umri wa miaka 23, na akaweza kukwepa kutiwa mbaroni.

Muungano wa Walinzi wa vitu vya thamani JSA, kampuni moja kubwa ya kibiashara, ilituma tahadhari kwa maduka yote yanayouza bidhaa na mapambo ya thamani kujihadhari na mwizi huyo sugu mapema miaka ya 70.
Rais wa kampuni hiyo kubwa alitaja tabia ya bi kizee huyo kama wizi au uhalifu wa aina yake.

Aidha anastaajabu kuwa angali anaiiba hata akiwa na umri huo mkubwa.
Akihojiwa na shirika la habari la Associated Press mwaka 2005, akiwa jela, bibi huyo Payne, alisema kuwa haibi kwa sababu ya pesa ila yeye hujikuta tu akiiba na haoni kama ataacha tabia hiyo, labda baada ya kufa.


Chanzo: BBC

DOGMATIC BLUSTERY WEATHER A POEM BY VENANCE GILBERT


Poem: Dogmatic Blustery Weather
Poet: Venance Gilbert
Composed September 27, 2015
Published on October 21, 2015.




The blustery weather blows wherever
By a hair's breadth in the oceans and ponds
Wind vane regularly measure the breeze.

The blustery weather has now turned to policies
Particularly in this phase of the GE
Propelling hard to the populations; the electorates
Populations frequently size them lyrics
Whichever the runners’ dogmas or troop expression.

It is the blustery weather since it blows to constituents
The dogmatic blustery weather will measured in the poll
Majority, make it take place on October
Be pacific under open and just environments.



ALL RIGHTS RESERVED.
Venance Gilbert © 2015

DOWNLOAD WIMBO MPYA: TOFA EMCEE-KUNG FU PANDA

Anaitwa Christopher Robert jina la kazi ya sanaa 'Tofa Emcee'.

 Tofa Emcee katika picha. Picha kwa hisani ya Facebook account Christoper TofaEmcee Robert

Donload Kung Fu Panda kwa kubofya HAPA.



BEN POL AELEZEA ALIVYONUSURIKA KIFO KATIKA AJALI YA BOTI


Msanii wa Bongo Fleva,Ben Pol amesimulia alivyonusurika kifo baada ya boti waliokuwa wakisafiria wakitokea visiwani Mbudya,jijini Dar kuzima ghafla katika ya bahari na kukaa kwa muda wa saa nzima bila kupata msaada.

Ben Pol alisema kuwa baada boti kuzima maji yalianza kuingia ndani  na engine ya boti ikazimika na boti hiyo ikaanza kuzama kilichowaokoa walikuwa wamevaa makoti ya kuogelea ‘life jackets’.

‘’Baada ya kukaa kwa saa nzima baharini kwa bahati nzuri ilipita boti ya wavuvi ikatuona ikatuokoa ila mmoja wetu hakuwepo kati ya tuliokolewa na hatujamuona ambao ni wanawake watatu, watoto hao walikuwa watatu, wanaume tulikuwa nane, lakini mmoja ndiye hatujui alipo.’alisema Ben Pol.

VAN VICKER AKUMBWA NA MAFURIKO AKIELEKEA KWAKE

Mafuriko makubwa yaliyoikumba jiji la Accra nchini Ghana usiku wa kuamkia juzi na kuleta maafa ya kuua watu 175 wakiwa wamejihifadhi kwenye kituo cha mafuta baada ya kituo hicho kulipuka moto,yamemkumba pia Staa wa filamu nchini humo Van Vicker akiwa barabarani akielekea nyumbani kwake.

Kupitia akaunti yake Instagram Van Vicker aliandika kuwa ameshuhudia mafuriko kwa macho yake (live),huku taa za barabarani zikiwa haziwaki,kuna mashimo,matakataka,umeme ukiwa umekatika na barabara zilikuwa zimefurika maji, na magari yalikuwa yameharibika.

Pia aliongeza kuwa waliokuwa wakitembea barabarani walikuwa wakitafuta pa kujihifadhi,madereva walipaniki na bado wakati huo mvua ilikuwa ikinyeesha na pia foleni ilikuwa kubwa na barabara ni ndogo.
Ambapo alisema kuwa kawaida huwa inamchukua dakika 45 kwenda nyumbani kwake lakini siku hiyo ilimchukua masaa sita kufika nyumbani kwake.


Chanzo; Udaku Specially

URUSI NA QATAR HUENDA ZISIANDAE KOMBE LA DUNIA

Mkuu wa kamati ya uhasibu wa shirikisho la soka duniani FIFA Domenico Scala amesema huenda Urusi na Qatar zikapoteza nafasi za kuyaandaa mashindano ya kombe la dunia mwaka 2018 na 2022 mtawalia iwapo ushahidi utaonyesha kulikuwa na ufisadi katika shughuli ya kinyanganyiro cha kupata kibali cha kuandaa mashindano hayo. Scala hata hivyo amesema mpaka kufikia sasa hawajapokea ushahidi wowote wa kudhihirisha kuwa nchi hizo mbili zilitoa hongo. Matamshi yake ndiyo ya kwanza kutolewa na afisa wa ngazi ya juu wa FIFA kuwa kuna uwezekano nchi hizo zikapokonywa uenyeji wa mashindano hayo. Maafisa wa idara ya mahakama wa Uswisi tayari wameanzisha uchunguzi kuhusu kutolewa kwa kandrasi hiyo ya kuandaa mashindano ya 2018 na 2022 kama sehemu ya uchunguzi wa madai ya ufisadi katika FIFA. 

Chanzo: DW

MKUTAO WA G7 KUANGAZIA USALAMA NA MAZINGIRA

Viongozi wa nchi tajiri zaidi duniani zinazounda kundi la G7 wanatarajiwa hii leo kutoa msimamo wa pamoja dhidi ya vitisho vya kiuslama vinavyoikumba dunia vikiwemo kitisho cha makundi ya wanamgambo wenye itikadi kali hadi kile Rais wa Marekani Barack Obama amelaani na kuutaja kama uchokozi wa Urusi nchini Ukraine. Kwa mara ya tatu mfululizo, viongozi hao wamemtenga Rais wa Urusi Vladimir Putin kutoka mkutano huo ulioanza hapo jana na unaokamilika hii leo katika mji wa Elmau nchini Ujerumani na badala yake wamewaalika viongozi kutoka kwingineko akiwemo waziri mkuu wa Iraq Haider al Abadi na Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari ambao wote wawili wanakabiliwa na kitisho kutoka makundi ya wanamgambo. Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Ufaransa Francois Hollande wanatarajiwa kuangazia masuala ya mazingira katika mkutano huo hasa kuongezeka kwa viwango vya joto duniani na athari zake.

Chanzo: DW

KOMBE LA DUNIA KWA WANAWAKE

Michuano ya kombe la dunia la wanawake,inaendelea huko canada katika miji tofauti tofauti.michuano hiyo ya kombe la dunia kwa wanawake liliendelea tena hapo jana kwa michezo miwili kupigwa kati ya Norway waliopepetana na Thailand.

Ujeruman ilioonesha kazi pwani ya samawati naizungumzia Ivory Coast na matokeo yalikuwa hivi Norway waliibuka na mtaji wa magoli manne huku Thailand wakikubali matokeo na kutulia na yai.

Kwa upande mwingingine kwenye mechi ya pili Ujerumani walijizolea magoli yao mawili na kuwaacha Ivory Coast mikono mitupu.

Chanzo: BBC

WATU 400 WAFARIKI KATIKA MTO YANGTSE

Meli iliyozama China
Msemaji wa serikali nchini China anasema kuwa karibu watu 400 wanahofiwa kuaga dunia wakati feri ilipozama kwenye mto Yangtze siku ya jumatatu.
Idadi hiyo imeongezeka kwa haraka baada ya makundi ya uokoaji kusaka vyumba vya feri hiyo.
Kwa sasa meli hiyo imendolewa majini kwa kutumia mitambo mikubwa.
Jumla ya watu 456 walikuwa ndani ya feri hiyo wakati ilipokumbwa na dhoruba ambapo ni watu 14 tu walioripotiwa kuponea ajali hiyo.
Ajali hiyo inaripotiwa kuwa mbaya zaidi nchini humo tangu miaka 60 iliyopita.



Chanzo: BBC

RAIS KIKWETE AELEKEZA NGUVU KATIKA ELIMU YA KIDATO CHA 5 & 6

Rais Jakaya Kikwete akipokea tuzo maalum kutoka kwa Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi, Dk.Shukuru Kawambwa kwa kutambua mchango wake katika kuendeleza na kuboresha elimu nchini wakati wa maadhimisho ya kilele cha wiki ya elimu yaliyofanyika katika uwanja wa michezo wa Jamhuri mjini Dodoma jana. Picha na Ikulu

Rais Jakaya Kikwete jana alitumia kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Elimu kuaga wadau wa sekta hiyo, akisema sasa nguvu zielekezwe katika kujenga majengo kwa ajili ya masomo ya elimu ya juu ya sekondari.

Rais Kikwete, ambaye alikiri kuwapo udhaifu katika kipindi cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Nne, alisema mafanikio pia ni makubwa kiasi kwamba sasa hakuna wanafunzi wanaokosa nafasi ya kwenda sekondari baada ya kufaulu na hivyo nguvu sasa inatakiwa kuwekwa katika kuongeza miundombinu ya kidato cha tano na sita.

Kikwete alitoa kauli hiyo jana kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini hapa alipohutubia maelfu ya wakazi wa Dodoma, wakiwamo wanafunzi wa shule za sekondari na msingi katika kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Elimu.

Rais alisema katika kipindi cha uongozi wake, amekuwa akitamani kutekeleza yale aliyoyaahidi bila ya kuacha jambo na akaongeza kuwa kuna haja ya kuongeza majengo kwa kidato cha tano na sita pamoja na kukamilisha majengo ya maabara.

Rais Jakaya Kikwete aliwataka wadau wa elimu na sekta binafsi kujenga shule za kidato cha tano na sita ili kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya elimu ambalo amelifikisha katika hatua nzuri katika kipindi chake cha miaka 10.

Kikwete, ambaye uongozi wake ulianzisha mkakati wa kujenga shule za sekondari za kata, alisema kwa sasa zipo za kutosha kumuwezesha kila mwanafunzi anayemaliza darasa la saba kupata nafasi ya kwenda sekondari kulingana na ubora na kiwango cha ufaulu wake.

“Ukiona mtoto amefeli, basi amefeli kweli na siyo kama zamani tulipokuwa tunasema hakuchaguliwa kwani nafasi zilikuwa chache. Hivi sasa anayefaulu kulingana na vigezo anapata nafasi hayo ni mafanikio makubwa katika elimu,” alisema Rais Kikwete.

Alifafanua kuwa hata bajeti ya elimu kwa miaka yake 10 aliyokuwa madarakani imekuwa ikiongezeka kila mwaka huku mwaka ya mwaka 2014/15 ikiwa kubwa kuliko miaka miaka iliyopita.

Alitoa mfano wa bajeti ya mwaka 2005/2006 wakati anaingia madarakani zilitengwa Sh669.5 bilioni wakati mwaka 2014/2015 zimetengwa Sh3.1 trilioni ili kuhakikisha kunakuwapo na elimu bora inayopatikana katika nyanja zote.

Alifafanua kuwa hata bajeti ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu imeongezeka kutoka Sh56.1 bilioni hadi Sh345 bilioni. Kwa sababu hiyo idadi ya wanafunzi wanaofaidika imeongezeka kutoka 16,345 mwaka 2005 hadi 98,000 mwaka 2014.  Huku shule za msingi zikiongezeka kutoka 14,257 mwaka 2005 hadi 16,343 mwaka 2014.

Pamoja na kusifia mambo mengi ambayo alisema yamefanywa na utawala wake, Rais alikiri kuwa bado kunahitaji kazi ya ziada katika kufanikiwa kielimu kama ilivyo kwa nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

“Tumefanikiwa katika mambo mengi kwenye elimu ingawa bado tunakabiliwa na changamoto. Kazi iliyopo mbele yetu ni kuhakikisha elimu inakuwa bora zaidi na kwa wote,” alisema JK.

“Tumefanya mambo mengi kwa pamoja. Nawaageni bai bai kwani sherehe zijazo mtakuwa na Rais Mwingine, mkitupa nafasi tena haya.”

Alisema mpango wa Tekeleza Matokeo Makubwa Sasa (BRN) aliutoa nchini Malaysia ambako alikuta kuna utaratibu wa kufuatilia masuala ya utekelezaji wa ahadi za Serikali.

“Wenzetu kule waliamua kuwafanyia mitihani walimu wao ili kujua kama kweli walikuwa na uelewa wa kile walichokuwa wanafundisha, walimu wengi walifeli hivyo wakagundua wanachokifundisha nao hawakijui,” alisema.

Kutokana na hilo, alisema kuwa Tanzania nao waliamua kuwapa mtihani walimu kwa baadhi ya masomo na kwamba nao walifeli.

Katika mkutano wa jana, Rais aliwatunuku vyeti na zawadi mbalimbali zikiwamo fedha wanafunzi na shule zilizofanya vizuri katika mitihani ya kumaliza darasa la saba na kidato cha nne 2014.

Nao Wizara ya Elimu waliamua kumtunuku Rais tuzo mbili ikiwemo ya uongozi bora na Weredi na Tuzo ya BRN, huku Mama Salma Kikwete akitunukiwa tuzo ya kumtunza Rais hadi kufikia kiwango cha kutekeleza majukumu yake ipasavyo ambapo alipewa ng’ombe wawili wa maziwa.



Chanzo: Mwananchi Communication Ltd

PINDA: CCM ITAELEZA HAYA KWENYE KAMPENI ZA UCHAGUZI MKUU

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, jana alihitimisha mjadala wa makadirio ya Bajeti ya Ofisi yake ya Sh trilioni 5.7 ambayo ilipitishwa na Bunge, huku akifafanua hoja zitakazotumiwa na CCM kuomba kura za wananchi katika Uchaguzi Mkuu ujao.


Pinda alisema hakuna haja ya kuandikia mate wakati wino upo na kufafanua kuwa katika Uchaguzi Mkuu, CCM itatakiwa kueleza mafanikio ya Serikali katika nishati ya umeme vijijini, miundombinu ya barabara, elimu, maji na afya.


Alitaka waliokuwa wakijiuliza nani atashinda katika uchaguzi huo, wapitie kidogo historia kuanzia mwaka 1995 mpaka katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, uliofanyika Desemba mwaka jana, ili waelewe nani alipata kipigo.


Elimu


Akifafanua kwa ufupi mafanikio yaliyopatikana katika elimu, Pinda alisema watakapoulizwa katika sekta hiyo nini kimefanyika, wataweka wazi kuwa ingawa bado kuna changamoto lakini yapo pia mafanikio makubwa.


“Wacha tubebe lawama katika changamoto, lakini tutaeleza kuwa katika vyuo vya ufundi mwaka 1995 na 1996, udahili katika vyuo vya ufundi ulikuwa 7,700 tu, mwaka 2005 wanafunzi 78,000 lakini takwimu za 2013, waliodahiliwa walikuwa wanafunzi 145,000,” alisema.


Katika vyuo vikuu, alisema mwaka 2005 walikuta vyuo vikuu vikiwa 23 lakini takwimu za 2013, zinaonesha kuwa vyuo vikuu vimefikia 50 na ongezeko hilo lisingewezekana kama si kuwepo kwa sera nzuri na usimamizi mzuri wa Serikali.


Kuhusu idadi ya wanafunzi waliodahiliwa katika vyuo hivyo, Pinda alisema mwaka 2005 walikuta wanafunzi 40,000 katika vyuo vikuu lakini mwaka 2015 wanaiacha nchi ikiwa na wanafunzi 200,000 waliopo katika vyuo vikuu mbalimbali.


Kuhusu ubora wa elimu aliosema kuwa una changamoto, lakini alikumbusha kuwa utafiti uliofanyika wa vyuo vikuu 100 bora Afrika, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM),kiliibuka namba nne kwa ubora Afrika na kufuatiwa na Chuo Kikuu cha Capetown Afrika Kusini.


Katika elimu ya msingi, alisema alipokwenda Marekani alipatwa na mshangao kukabidhiwa Tuzo ya Maendeleo ya Umoja wa Mataifa katika Uandikishaji wa Wanafunzi wa Elimu ya Msingi.


Afya


Katika sekta ya afya, Pinda alisema umri wa kuishi wa Mtanzania umeongezeka huku vifo vya watoto chini ya miaka mitano vikipungua. “Tanzania ni miongoni mwa nchi tano barani Afrika, zilizofanya vizuri katika kupunguza vifo vya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano,” alisema.


Miundombinu ya barabara


Kuhusu miundombinu ya barabara, Pinda alihoji ni nani anayeweza kusimama kwa wananchi na kusema Serikali haijafanya chochote katika sekta hiyo.


“Hivi kuna anayeweza kusema kuwa katika barabara hatujafanya kitu na akasimama kwa wananchi kuomba kura? Njooni kule Rukwa nenda Kigoma useme hakuna kitu, nawahakikishia hamtapata kura,” alisema.


Aliwasema wabunge wa Kigoma ambao tangu Uhuru wamekuwa wakilalamika kuwa mkoa huo umetengwa na kushangazwa kwa hatua yao ya kutosema chochote kuhusu ujenzi mkubwa wa barabara kwenda katika mkoa huo na daraja kubwa la Kikwete.


Mbali na Daraja la Kikwete, Pinda alisema madaraja zaidi ya 20 yaliyokuwa kikwazo katika miundombinu ya barabara yamejengwa huku vivuko vingi katika mito, maziwa na bahari vikinunuliwa.


Maji, umeme


Kwa upande wa huduma ya maji, Pinda alisema kuna kazi kubwa imefanyika katika miaka miwili iliyopita na kutoa mfano wa Mradi wa Maji Karatu.


“Inasikitisha hata rafiki yangu wa Karatu akija hapa hasemi mradi huu ni mzuri. Wamejenga shule nzuri lakini hawasemi, lakini mimi nilipofika pale niliwasifia shule nzuri kwa kuwa najua wanatekeleza Ilani ya CCM,” alisema Pinda.


Kuhusu umeme vijijini, Pinda alisema ingawa hawajamaliza vijiji vyote lakini kazi imefanyika na kwa kuwa anaamini kuwa Serikali ijayo ni ya CCM, kazi hiyo itaendelezwa na Serikali ijayo.Kilimo
Katika kilimo, Pinda alisema changamoto kubwa iliyokuwa ikisumbua Taifa ilikuwa kukosekana kwa usalama wa chakula, jambo alilosema ilikuwa aibu kwa taifa kuomba chakula nje ya nchi.

Alisema Serikali ya Rais Jakaya Kikwete, imejitahidi na leo Tanzania inatamba kuwa hata mikoa yenye njaa, italishwa kwa kutumiachakula kilichozalishwa ndani ya nchi.

AlisemaTanzania ni nchi ya nne barani Afrika kwa kuzalisha mahindi, duniani inashika nafasi ya 12 katika uzalishaji wa zao hilo huku akiongeza kuwa mwaka 2005 kulikuwa na matrekta 4, 000, sasa matrekta yaliyopo ni zaidi ya 10,000.

“Tusingewekeza katika uzalishaji wa mazao ya kilimo, tusingekuwa na jeuri ya kulisha mikoa yote yenye njaa. Kwa sasa tunaweza kulisha hata nje ya nchi na hivi karibuni, Sudan walikuja kuomba tuwasaidie. “Hata Kenya mwaka jana walikuja kuomba tuwasaidie tani 240,000 na tukawapa…nasema lazima tuone jeuri katika hilo,” alisema Pinda.

Uchumi


Pinda alisema yapo mambo mengi yanafanyika katika uchumi wa nchi na kutoa mfano wa utafiti wa wataalamu wa Benki ya Dunia (WB) wa mwaka 2012 kwa kushirikiana naTaasisi ya Business Insider kuhusu nchi zenye uchumi unaokua kwa kasi.

Kwa kutumia vigezo vya ukuaji wa uchumi, Pinda alisema utafiti huo ulikuja na nchi 29 duniani ambazo zina uchumi unaokua kwa kasi na Tanzania ilishika namba 15.

Mbali na utafiti huo, mwingine ulifanywa na taasisi ya KPMJ ya Afrika Kusini kutafuta nchi kumi zenye uchumi unaokuwa barani Afrika na Tanzania ikashika nafasi ya sita.

Pia alitaja utafiti wa kikanda uliofanywa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) Aprili mwaka huu, ikabainishwa kuwa Tanzania inafanya vizuri. “Katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, sisi ndio tunaong’ara na hata hao watafiti wakija wanaona viashiria vilivyo bayana kabisa vya ukuaji wa uchumi,” alisema Pinda.

Alitoa mfano wa Mkoa wa Dodoma, kwamba alipokuwa anakuja na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere miaka ya 1980 na mkoa huo ulivyo sasa ni vitu viwili tofauti.

Ujenzi wa madarasa Pinda alisema anajua mafanikio hayo lazima yawaume Kambi ya Upinzani kwa kuwa wamenyang’anywa hoja za kuwaeleza wananchi katika uchaguzi mkuu.

Alisema hata kama inawauma hivyo, lakini ni vyema wanapojadili waheshimiane kuliko ilivyokuwa wakati wa kujadili makadirio ya Bajeti ya ofisi yake, ambapo baadhi ya wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani, walifikia hatua ya kuacha kuheshimiana na kuwaita mawaziri hawana akili.

“Ah! Inaonekana upande huo mna akili sana, lakini hivi Mbowe mkija kushika madaraka na sisi tukakaa huko tuache kuwaheshimu mtafurahi? Msiwatendee wenzenu lile msilopenda kutendewa,” alisema Pinda.

Alimtaka Mbowe na kundi lake la Umoja wa Katiba ya Wananchi(UKAWA), katika mikutano yao ya kuchangisha fedha, wajaribu hata kujenga darasa moja ili wajue anachozungumzia cha kushirikiana na wananchi katika kuleta maendeleo nini maana yake.



Chanzo: Habari Leo

RAIS NKURUNZINZA KULIPIZA KISASI KWA WAASI



 Burundi Pierre Nkurunziza amewapongeza wanajeshi wazalendo waliozuia mapinduzi na kurejesha hali ya usalama na utawala huru mjini Bujumbura.

Rais Nkurunziza amewataka waburundi wazalendo kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi utakaofanyika mwezi juni.

Rais huyo alikuwa Mjini Dar es Salaam Tanzania siku ya Jumatano kuhudhuria mkutano wa viongozi wa kanda ya Afrika Mashariki kundi la wanajeshi waasi walipotangaza ''Mapinduzi'' dhidi ya serikali yake.

Viongozi watatu miongoni mwa makamanda 6 wa jeshi waliounga mkono tangazo hilo la ''mapinduzi'' ilikupinga muhula wa tatu wa rais huyo tayari wamekamatwa.

Kufikia sasa watu 105,000 wameripotiwa kutorokea mataifa jirani kulingana na takwimu za Umoja wa Mataifa.

Baada ya kurejea kutoka Tanzania rais Nkurunzinza alielekea Kaskazini mwa Bujumbura eneo alikotokea kabla ya kurejea katika kasri la rais lililoko katika mji mkuu wa Bujumbura.
Katika taarifa iliyochapishwa mtandaoni rais Nkurunzinza alisema kuwa ''
kuna amani na utangamano katika asilimia kubwa ya Burundi na hata katika mji mkuu wa Bujumbura ila tu watu wachache waasi ndio waliokuwa na hamu ya kuvuja damu''
''Jeshi la taifa lilionesha ukomavu wake lilipokabiliana na wasaliti hao''

''Ningependa kuwahimiza waburundi wazalendo walinde kwa dhati amani iliyoko sasa kwani ndio ngao na msingi wa demkrasia iliyoko Burundi''
''Shari msingi wa demokrasia yetu changa ilindwe isiyeyuke''
Nkurunziza aliahidi kulipiza kisasi dhidi ya ''yeyote aliyejaribu kuwasha moto wa uhasama baina ya waburundi''

Nkurunziza aliahidi kulipiza kisasi dhidi ya ''yeyote aliyejaribu kuwasha moto wa uhasama baina ya waburundi''
Rais Nkurunzinza aliwasili mjini Bujumbura Ijumaa akiwa ameambatana na maelfu ya wafuasi wake.

Mwandishi wa BBC aliyeko huko Ruth Nesoba anasema japo asilimia kubwa ya mji huo ulikuwa na amani, katika sehemu zingine kulikuwa na waandamanaji walioweka vizuizi barabrani wakipinga kuwania kwake kwa muhula wa tatu.

Polisi wa kupambana na ghasia walikuwa wakikabiliana nao kwa kuwafyatulia mabomu ya kutoa machozi.

Miongoni mwa makamanda waliokamatwa kwa kuchochea uasi ni pamoja na waziri wa zamani wa ulinzi Cyrille Ndayirukiye.

Makamanda watatu waliotangaza ''Mapinduzi'' wamekamatwa
Waziri wa sasa wa usalama Gabriel Nizigama aliiambia BBC kuwa maafisa wawili wakuu katika idara ya polisi pia walikamatwa pamoja na wadogo wao takriban 12 waliokuwa wakiwalinda.
Wawili hao walikamatwa baada ya ufyatulianaji wa risasi nje ya jumba walimokuwa
.
Kiongozi wa uasi huo meja jenerali Godefroid Niyombare,aliyetangaza ''mapinduzi'' hayo siku ya jumatano hajakamatwa japo alinukuliwa na shirika la habari la AFP akisema kuwa atajisalimisha.

''Nitajisalimisha kwa utawala, natumai hawataniua'' alisema meja jenerali Niyombare.

JACKLINE WOLPER ANASWA LIVE AKITOKA JUMBA LA FREEMASONS

Mshtuko! Staa wa sinema za Kibongo, Jacqueline Wolper Massawe ameibua maswali kwa mashuhuda walimuona ‘live’ akiingia kwenye hekalu la watu wa Jamii ya Siri (Secret Society) ya Freemasons yenye nguvu duniani inayohusishwa na imani za kishetani.

TUJIUNGE MTAA WA SOKOINE
Tukio hilo lililoibua kizaazaa kwa mashuhuda waliomuona Wolper, lilijiri juzikati, mishale ya jioni kwenye hekalu hilo lililopo Mtaa wa Sokoine mkabala na Hoteli ya Hyatt Regency, The Kilimanjaro jijini Dar jirani na Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

SIMU ZAMIMINIKA
Likiwa kwenye majukumu ya kusaka habari kama kawaida yake, gazeti hili lilipokea simu kadhaa kutoka kwa mashuhuda hao wakiwataka wanahabari wetu kuwahi eneo la tukio.
Kufuatia umbali waliokuwa mapaparazi wetu, ilibidi kuwaomba mashuhuda hao ‘kumfotoa’ picha ambapo mmoja wao alifanya hivyo na kuziwasilisha kwenye meza ya gazeti hili.

ALINASWAJE?
Akidadavua mazingira aliyonaswa Wolper, shuhuda huyo alikuwa na haya ya kusema:
“Kwanza mwanzoni hatukumjua kama ni Wolper lakini kuna dada ambaye anamjua vizuri na ni shabiki wake mkubwa ndiye aliyetuhakikishia kuwa ni Jacqueline (Wolper).

“Kuna waliomuona akiingia. Nilipofika mimi nilimkuta getini anatoka. Walisema hakukaa muda mrefu kwani alitumia dakika kadhaa kisha akatoka na kwenda kwenye gari lake aina ya Prado (Toyota) alilopaki mbali kidogo na lango hilo,” alisema shuhuda huyo kwa sharti la kutotajwa jina na kuongeza:
“Baada ya hapo alitoka nduki maana nzi (watu) walikuwa wameanza kumjalia na kulizingira gari lake.”

WOLPER AJITETEA
Baada ya kuzikagua picha za Wolper akiwa katika mazingira hayo na kujiridhisha kuwa ni yeye, gazeti hili lilimbana mwigizaji huyo ambapo alijitetea:

“Jamani nilikuwa sina hili wala lile. Kuna jengo nilikuwa nalitafuta ndiyo nikajikuta nimetokea maeneo hayo.
“Mimi mwenyewe nilishtuka kuona watu wananiangalia sana kumbe ndiyo nikagundua nipo kwenye lango la Freemasons.”
Risasi Jumamosi: Mbona kuna mashuhuda walikuona wakati unaingia na wakati unatoka?
Wolper: Unajua mimi sikuona kibao chao lakini sikuingia kabisa hadi kule ndani.

Risasi Jumamosi: Lakini kuna madai kwamba wewe ni mwanachama. Unasemaje?
Wolper: Mimi siyo Freemasons, nakumbuka kuna siku watu walinifuata wakaniambia nijiunge Freemasons nitakuwa na mafanikio lakini sijakubaliana nao.

TUJIKUMBUSHE
Mwaka 2012 wakati wa kifo cha aliyekuwa mwigizaji mkubwa Bongo, marehemu Steven Kanumba ‘The Great’ kuliibuka madai ya baadhi ya wasanii ambao ilisemekana ni ‘memba’ wa Freemasons

Mbali na Kanumba, wengine waliotajwa kwenye listi hiyo mwaka huo alikuwepo Wolper na mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ ambaye madai hayo yamekuwa yakiendelea kumganda huku wengi wakiwa na imani potofu kuwa ukijiunga na jamii hiyo unapata utajiri wa ghafla.

Source:Global Publishers

HABARI LEO TAHARIRI: TFF IFANYIE KAZI KASORO ZA MSIMU ULIOMALIZIKA

MSIMU wa Ligi Kuu Tanzania Bara umemalizika Jumamosi iliyopita, huku timu za Polisi Morogoro na Ruvu Shooting ya mkoani Pwani zikishuka daraja.

Kushuka kwa timu hizo mbili kunatoa nafasi kwa timu nne kupanda daraja kukiwa na lengo la kuongeza timu shiriki kutoka 14 hadi 16 katika msimu ujao wa ligi hiyo.

Timu zilizopanda daraja ni Majimaji ya Songea, African Sports ya Tanga, Toto African ya Mwanza na Mwadui ya Shinyanga, ambazo zinakamilisha timu hizo nne.

Wakati msimu huo wa ligi ukifungwa, tayari Yanga na Azam FC walishajitangazia nafasi za kwanza na pili na kuwa na uhakika wa kuliwakilisha taifa katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa na ile ya Shirikisho la Afrika.

Baada ya kumalizika kwa msimu huu wa ligi ndio mwanzo wa msimu unaokuja na timu zinatakiwa kujipanga vizuri kwa ajili ya msimu huo, ambao kama baadhi ya makosa yatarekebishwa, inaweza kuwa ligi bora zaidi.

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), timu pamoja na wadau wengine wa ligi hiyo kama kamati mbalimbali, ambazo kwa njia moja ama nyingine zinahusika katika kuendesha ligi hiyo, zinatakiwa kufanya tathmini kwa yale yaliyopita.

Hakuna ubishi kuwa pamoja na kutojali uwezo wa kifedha, timu zilijitahidi sana hata zile ambazo hazina majina makubwa zilifanya vizuri uwanjani na kuvitoa jasho vigogo.

Lakini pamoja na uzuri wa msimu huo, bado kuna changamoto kibao zilizojitokeza, ambazo kwa kiasi fulani zilitia doa ligi hiyo, ambayo angalau ilikuwa na wadhamini waliosaidia timu kutoa lia njaa kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

TFF wakati umefika sasa wa kuwa makini wakati wa upangaji wa ratiba na lazima mzingatie mazingira ya mikoa pamoja na miundo mbinu ya nchi yetu, ili kuziwezesha timu kucheza mechi zao bila tatizo.

Timu nyingi zililalamikia ratiba ambayo haikuwa rafiki kwani utakuta timu inacheza mchezo mmoja katika mkoa fulani ambao una timu zaidi ya moja halafu inaondoka na kurudi tena baadaye na kuzisababishia usumbufu na gharama zisizo za lazima.

Mfano mkoa wa Mbeya una timu mbili, hivyo timu ilitakiwa angalau inapokwenda icheze mechi zote mbili na ndipo iende mahali pengine ili iweze kubana matumizi na kutumia muda vizuri.

Mbali na kasoro hiyo ya upangaji mbovu wa ratiba, pia kulikuwa na kasoro zingine kama baadhi ya waamuzi kuchezesha ama kwa upendeleo au chini ya kiwango kwa kutojua sheria 17 za soka, ambazo ni muhimu.

Timu nyingi hasa zile ndogo zililalamikia sana waamuzi na wengi walidai kuwa walikuwa wakiumwa kwa makusudi ili kuzibeba timu kubwa na kuzipatia matokeo mazuri kwao.

TFF na wadau wengine wote wanatakiwa kujifunza kutokana na makosa ya msimu uliopita ili kuuboresha msimu ujao na kuifanya Ligi Kuu Bara kuwa ligi bora zaidi.

Ligi bora hutoa timu bora ya taifa, hilo halina ubishi, hivyo ni jukumu la TFF kuhakikisha ligi inakuwa bora ili kupata timu bora ya taifa itakayofanya vizuri katika mashindano ya kimataifa.

Chanzo: Kutoka Bodi ya Uhariri Gazeti la Habari Leo.