Showing posts with label Celebrity. Show all posts
Showing posts with label Celebrity. Show all posts

MFAHAMU WOLE SOYINKA GWIJI WA FASIHI YA KIAFRIKA MWENYE TUZO YA NOBEL KATIKA FASIHI 1986

Picha kwa hisani ya Oasis Magazine

Bila shaka jina la Wole Soyinka sio geni masikioni mwako kwa sababu wengi wetu tumesoma tamthiliya (play) yake ya The Lion and The Jewel sekondari hasa kidato cha tatu na cha nne na The Trials of Brother Jero kwa wale waliosoma miaka ya nyuma.

Hapa nitamzungumzia Wole Soyinka, mwafrika wa kwanza kushinda tuzo ya Nobel katika fasihi. Haya ni mambo ambayo huwezi kufundishwa kwenye mitaala ya shuleni, hivyo unapaswa kuyafahamu nje ya mtaala wa shule kwa muda wako mwenyewe. Awali ya yote, ni kwamba wasifu huu niliuandika kwa mara ya kwanza katika mtandao wa Twitter Julai 13, 2020 kabla sijaamua kuuleta hapa.


MAISHA YA MWANZO

Soyinka alizaliwa Julai 13, 1934 huko Abeokuta jirani na Ibadan nchini Naijeria. Majina yake halisi ni Akinwande Oluwole Babatunde Soyinka lakini anafahamika sana kama Wole Soyinka. Alisoma Fasihi, Ibadan. Mwaka 1954 alijiunga na Chuo Kikuu cha Leeds nchini Uingereza mara baada ya kumaliza masomo yake katika Chuo cha Serikali, Ibadan. Katika kipindi cha miaka 6 aliyokua Uingereza alikua akiandika na kuongoza uigizaji wa tamthiliya za majukwaani katika kampuni ya Royal Court Theatre mwaka 1958-1959. Akiwa hapo chuoni aliwahi kua mhariri wa jarida maarufu la chuoni hapo la The Eagle. Mwaka 1960 alifadhiliwa na taasisi ya Rockefellers kurudi nchini Naijeria kwa ajili ya kuifanyia utafiti tamthiliya ya Kiafrika katika chuo Kikuu cha Ibadan wakati huo kiitwa University College, Ibadan.

Amewahi kufundisha tamthiliya na fasihi katika Vyuo Vikuu vya Obafemi Owolowo (zamani Ife), Ibadan na Lagos ambapo mwaka 1975 alikua Profesa wa Fasihi Linganishi (Comparative Literature). Mwaka 1960 Soyinka alianzisha kundi la sanaa za jukwaani la The 1960 Masks na mwaka 1964 akaunda kampuni aliyoiita The Orisun Theatre Company. Kote alizalisha tamthiliya zake na pia alishiriki kama muigizaji. Lakini pia mwaka 1957 aliwahi kuwa mshiriki na mhariri katika jarida la Black Orpheus ambalo lilikua likichapisha kazi za washairi wa Afrika kama Christopher Okigbo wa Naijeria, Dennis Brutus na Alex La Guma wa Afrika ya Kusini pamoja na Tchicaya U Tam'si wa Kongo Brazzaville.


MSUKUMO KATIKA KAZI ZA FASIHI

Soyinka alivutiwa sana na uandishi wa John Millington Synge mwandishi wa Ireland, lakini alipenda sana kuzilinganisha kazi zake na utamaduni wa maigizo ya Afrika akichanganya na muziki, dansi pamoja na vitendo (uigizaji). Pia uandishi wake uliegemea katika masimulizi yaliyohusisha utamaduni wa kabila la Yoruba uliolenga hasa kumzungumzia Ogun ambaye ni mungu wa kabila hilo. Aliandika tamthiliya yake ya kwanza inaoitwa The Swamp Dwellers (1958) akiwa nchini Uingereza ambayo iliigizwa huko Ibadan 1958 na The Lion and the Jewel iliyoigizwa 1959, hizi zote zilichapishwa mwaka 1963.


TAMTHILIA

The Lion and the Jewel imekua ikifundishwa kwa muda mrefu sana katika somo la fasihi ya kiingereza hapa chini. Mchezo huu ni mchezo wa kuchekesha kuhusu mgongano kati ya maadili ya jadi ya Kiafrika na athari za ustaarabu wa kisasa wa Magharibi. Katika tamthilia nzima, Soyinka anagusia mada za mila dhidi ya usasa, nafasi ya wanawake katika jamii, na utata wa upendo na tamaa. Vipengele vya ucheshi vya tamthilia hii huifanya kuwa ya kuburudisha na kusisimua, kwani inatoa ufafanuzi kuhusu mivutano inayoendelea kati ya mila na mabadiliko katika Afrika ya baada ya ukoloni.

Picha kwa hisani ya Amazon

Miongoni mwa kazi zake nyingine ni pamoja na The Trials of Brother Jero (1963) ambayo iliwahi kutafsiriwa katika lugha ya Kiswahili kama "Masaibu ya Ndugu Jero" na A. S. Yahya. Pia aliandika Jero's Metamorphosis (1973) ambao ni muendelezo. Hizi ni tamthilia za kejeli zinazomhusu mhusika Ndugu Jeroboamu, anayejulikana kama Ndugu Jero. Tamthilia hizi zinaeleza kuhusu matendo ya ufisadi ya baadhi ya viongozi wa dini na wepesi wa wafuasi wao. Kwa pamoja, tamthilia hizi hutoa ukosoaji mkali wa taasisi za kidini na kisiasa katika jamii za Kiafrika baada ya ukoloni. Soyinka anetumia ucheshi na kejeli kutoa mwanga juu ya ghiliba, unafiki, na unyonyaji ulioenea katika mifumo hii.

Picha kwa hisani ya Amazon

Vingine ni A Dance of the Forests (1973), Kongi's Harvest (1967) na Madmen and Specialists (1971) hivi viliigizwa majukwaani kwa kufikisha ujumbe kama kejeli kwa kutumia ucheshi kwa walengwa ambao ulikuwa ni utawala wa kijeshi nchini Naijeria kwa wakati huo. Miaka niliyoandika kwenye mabano ni muda ambao kitabu husika kilichapishwa na sio uigizwaji jukwaani.

Picha kwa hisani ya Amazon

Zipo tamthilia ambazo hazikuwa na kejeli kama vile The Strong Breed (1963), The Road (1965), The Bacchae of Euripides (1973) na Opera Wangosi (1981). Vitabu vingine alivyoandika ni Play of Giants (1984), Requiem for Futurologist (1985), Camwood on the Leaves (1960), Before the Blackout (1960), Death and the King's Horseman (1975) , From Zia, with Love (1992), The Beatification of Area Boy (1995), King Baabu (2001), Etiki Revu Wetin (2005), Alapata Apata (2011) na vitabu vingine vingi.


RIWAYA

Soyinka ameandika riwaya tatu: The Interpreters (1965) ambayo hadithi yake inawakutanisha wasomi kadhaa wa Naijeria: Egbo, Sekoni, Kola, Sagoe na Bandele wanaozungumzia kuhusu Uafrika na hasa kuikomboa nchi yao katika rushwa na mengine yasiyofaa. Wasomi hao wanajaribu kuangalia mabadiliko katika jamii yanayokuja kwa kasi hasa kusahaulika mila,desturi na tamaduni za kiafrika na ushawishi wa utamaduni wa Magharibi na Elimu.

Picha kwa hisani ya Amazon

Nyingine ni Season of Anomy (1973) Hii anazumngumzia mawazo yake yeye kama mwandishi. Anagusia nafasi ya mtu mmoja mmoja katika kuleta mabadiliko kwenye jamii ilijawa na uovu na mmomonyoko wa maadili hasa rushwa. Ina wahusika wachache tu ambao wanachukua hatua kupambana na jamii ya Naijeria iliyojaa rushwa na mmomonyoko wa maadili.

Picha kwa hisani ya Amazon

Riwaya ya tatu ni Chronicles from the Land of the Happiest People on Earth (2020). Riwaya hii ni kejeli hasa ikizungumzia masuala ya kisiasa na kijamii katika jamii ya sasa ya Naijeria. Riwaya hii inazungumzia kuhusu rushwa ambayo ni tatizo hasa katika nchi za Afrika, usaliti wa kisiasa na matatizo mengine ya kijamii yanayoikabili Naijeria ya sasa. Jina la kitabu tu ni kejeli tosha kuhusu jinsi jamii ya nje inavyoichukulia Naijeria na uhalisia halisi wa yanayoendelea nchini humo. Soyinka anatumia kejeli, ucheshi na uchunguzi wa kina kuelezea hali halisi katika nchi za Afrika. Riwaya hii inasadifu mambo mengi ambayo nchi za Afrika zimepitia hasa baada ya ukoloni. 

Picha kwa hisani ya Amazon


TAWASIFU

Tawasifu (autobiography) ni masimulizi yanayoandikwa na msanii mwenyewe kumhusu yeye mwenyewe. Hii ni tofauti na wasifu (bibliography) ambayo ni mmasimulizi kuhusu maisha ya mtu yanayoandikwa na mtu mwingine. Tawasifu hizo ni The Man Died: The Prison Notes of Wole Soyinka (1972). Katika tawasifu hii ambayo ni kama insha, Soyinka anaelezea maisha yake ya gerezani ambako alitiwa nguvuni kwa kujaribu kuilingilia mazungumzo wakati wa vita ya Biafra. Kitendo hiko kikapelekea kutiwa nguvuni na kuwekwa jela kwa miezi 27 kati ya mwaka 1967-1969 bila hukumu na kutiwa hatiani. Soyinka anaelezea maisha yake akiwa gerezani hasa ukatili aliofanyiwa, vitendo vinavyokizana na haki za binadamu, unyanyasaji wa kisaikolojia na migongano na maofisa wa gereza, walinzi na wafungwa wenzie katika gereza la Gowon.

Picha kwa hisani ya 4Sahadows Books

Tawasifu nyingine ni Aké: The Years of Childhood (1981) ambayo inaelezea maisha yake ya utotoni hadi kufikia miaka 11. Humo anaelezea maisha yake katika familia yake, utamaduni wa jamii ya Yoruba, kipindi cha ukoloni na nyakati ambazo zimetengeneza maisha ya mmoja wa waanshishi wa fasihi ya kiafrika. Soyinka anaelezea matukio ya utotoni mwake kujaribu kuelewa maisha ya ukubwani, matukio na vijana wa umri wake (peer) na jitihada za kufamu mazingira na mji wa Ake ambako ndiko alikozaliwa na kuishi. Mji huu uliopo Magharibi mwa Naijeria.

Picha kwa hisani ya Amazon

Tawasifu nyingine ni Ìsarà: A Voyage around "Essay" (1989). Tawasifu hii ameielekeza (dedicated) kuwa kumbukumbu ya baba yake ambaye amemuita jina la Essay. Kitabu hiki ni mjumuisho wa masimulizi na hadithi kumhusu baba yake na kipindi cha ukoloni nchini Naijeria.

Picha kwa hisani ya Amazon

Nyingine ni You Must Set Forth at Dawn (2006). Tawasifu hii ni muendelezo wa ile ya awali "Aké". Humo anaelezea maisha yake ya ukubwani, nafsi yake katika harakati za kisiasa nchini Naijeria kipindi alichoshikiliwa gerezani na maisha yuhamishoni (exile) na muingiliano na wanasiasa. Tawasifu nyingine ni Ibadan: The Penkelemes Years: a memoir 1946-65 (1994)

Picha kwa hisani ya Amazon

 

INSHA

Ameandika insha kadhaa ambazo ni Myth, Literature and the African World (1975). Humu anaelezea nafsi ya hadithi katika fasihi ya kiafrika akiilinganisha na tamaduni za Magharibi na kuelezea mtazamo wake kuhusu mtazamo mpana wa kiafrika kupitia masimulizi na hadithi.


Picha kwa hisani ya Amazon

Nyingine ni Art, Dialogue, and Outrage: Essays on Literature and Culture (1993). Huu ni mjumuisho wa mada mbalimbali kuhusu utamaduni wa Afrika, uhalisia wa maisha baada ya ukoloni, na nafasi ya fasihi katika jamii. Inajumuisha pia namna Soyinka anapokea uhakiki na ukosoaji wa kazi zake pamoja na mazungumzo na waandishi wengine.

Picha kwa hisani ya Amazon

Insha nyingine ni Of Africa (2012). Humu anaelezea historia ya Afrika, tamaduni, changamoto na nafasi ya barabla Afrika katika masimulizi. Anajadili mada kama vile dini, siasa na utambulisho (identity).

Picha kwa hisani ya Amazon

Insha nyingine ni The Burden of Memory The Muse of Forgiveness (1999) ambapo anaelezea kuhusu mabadiliko ya kisiasa na kijamii baada ya ukoloni akijikita zaidi katika changamoto za kumbukumbu na historia za matukio ya ukoloni, na kuwepo haja ya kusameheana na kupatana.

Picha kwa hisani ya AmazonPia ameandika Climate of Fear (2004) ambayo ni mjumuisho wa mihadhara (lectures) alizoziwasilisha katika jukwaa la BBC Reith Lectures. Humo anazungumzia kuhusu hali ya hofu na wasiwasi ulimwenguni baada ya tukio la kigaidi la Septemba 11 huko Marekani, matokeo ya tukio hilo kwa jamii na mtu mmoja mmoja. Anazungumzia ugaidi na ukandamizaji wa kisiasa unavyochochea hali ya hofu. Anaeleza namna hofu inavyoweza kutumiwa kama dhana ya kukandamiza siasa za upinzani, kuminya uhuru wa kutoa maoni nakadhalika.

Picha kwa hisani ya Amazon

Insha nyingine ni Beyond Aesthetics: Use, Abuse, and Dissonance in African Art Traditions (2019). Hii inaakisi nafasi ya sanaa na muingiliano wake na siasa na taaluma nyingine ikizama zaidi katika maisha ya Soyinka na mtazamo mpana kuhusu sanaa za utamaduni wa Afrika.

Picha kwa hisani ya Amazon


USHAIRI

Licha ya kuwa umaarufu wa Soyinka unatokana na uandishi wa tamthilia hayuko nyuma pia katika ushairi. Miongoni mwa vitabu vya vya ushairi ni Idanre and Other Poems (1967). Hiki ni kitabu chake cha mwanzo cha mashairi. Chimbuko la kitabu hiki ni eno le Idanre ambayo ni sehemu ya muhimu katika masimulizi ya utamaduni wa jamii ya Yoruba kwa vile kinagusia sana tamaduni na simulizi za huko.

Picha kwa hisani ya Amazon

Kingine ni A Shuttle in the Crypt (1972) ambacho alikiandika wakati akiwa gerezani kipindi cha vita ya Biafra. Dhamira za mashairi yake ni kuhusu kutengwa, mateso na uvumilivu katika kipindi kigumu.

Picha kwa hisani ya Amazon

Kitabu kingine ni Ogun Abibiman (1976) hii ni mojawapo ya kazi zake nyingi zinazomuenzi mungu wa Yoruba, Ogun. Ogun ni mungu wa chuma, vita, na ubunifu, na anashikilia nafasi muhimu katika masimulizi na  ya Kiyoruba. Soyinka ambaye ana ibada ya kibinafsi kwa Ogun, mara nyingi humwomba mungu katika kazi zake kama ishara ya ubunifu, mabadiliko, na mapambano yaliyomo katika uzoefu wa mwanadamu. Katika shairi hili Soyinka anachanganya Kosmolojia ya Kiyoruba na kisiasa na kijamii. mapambano ya Afrika. "Abibiman" ni neno linalorejelea Afrika. Shairi linaangazia changamoto zinazolikabili bara la Afrika, hitaji la umoja, na tumaini la kufufuliwa upya na mabadiliko. Shairi hili ni wito wa kuchukua hatua na maombolezo, likiangazia tofauti za Afrika baada ya ukoloni - urithi wake tajiri na changamoto zake za kisasa. Uelewa wa kina wa Soyinka wa mila za Kiyoruba na ushiriki wake wa kina na hali halisi ya Afrika baada ya ukoloni unakutana " Ogun Abibiman," na kuifanya tafakari ya kuhuzunisha juu ya siku za nyuma, za sasa na zijazo za bara.

Picha kwa hisani ya Goodreads

Pia ameandika Mandela's Earth and Other Poems (1988). Mjumuisho wa mashairi katika kitbu hiki yalikuwa ni mahsusi kwa Nelson Mandela, kiongozi na mpigania haki dhidi ya sera ya ubaguzi nchini Afrika Kusini. Pia kinazungumzia kuhusu uhuru wa watu, uthabiti na udhalimu. 

Picha kwa hisani ya Amazon

Soyinka aliandika Samarkand and Other Markets I Have Known (2002). Katika ushairi huu Soyinka aliakisi maeneo aliyotembelea na mambo aliyoyaona.

Picha kwa hisani ya Amazon

Pia aliandika Early Poems (1998). Kitabu hiki ni mjumuisho wa mashairi ya mwanzo kabisa ya Soyinka. Katika kitabu hiki mashairi yanasadifu historia ya Naijeria, utamaduni, siasa na maisha baada ya ukoloni. Pia ameandika Poems from Prison" (1969)

Picha kwa hisani ya Amazon


FILAMU

Soyinka amewahi kuandika na kuongoza filamu Blues for a Prodigal (1984) hii ni filamu ambayo Soyinka alihusika katika uandishi na uongozaji. Filamu hii ina muundo wa baadhi ya vipengele vya kazi za awali za Soyinka na uzoefu wake wakati wa Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Nigeria. Inahusu mtu mpotevu anayerejea katika mji wake na kuangazia mada mbali mbali za kijamii na kisiasa kwa kuzingatia ukosoaji wa Soyinka kuhusu jamii ya Nigeria.

Ingawa filamu hii haitambuliwi sana au kujadiliwa kwa upana kama kazi nyingine nyingi za Soyinka bado inasimama kuonesha umahiri wake katika mambo mengi na kujiingiza kwake katika tasnia ya filamu na kuleta mtindo wake wa kipekee wa masimulizi na masuala ya dhamira kwa hadhira tofauti.


TUZO, HESHIMA NA SIFA

Soyinka ametunukiwa tuzo nyingi sana kutokana na uandishi wake hasa wa tamthilia na harakati zake katika demokrasia na haki za binadamu. Tuzo hizi ni kuanzia nchini mwake Naijeria na kimataifa. Ametunukiwa tuzo nyingi na kutajwa katika tuzo nyingi. Hizi ni baadhi ya tuzo na heshima alizotunukiwa:

(i) Tuzo ya Nobel katika Fasihi (1986). Hii ni tuzo ya maarufu ambayo Soyinka amewahi kutunukiwa na kuwa Mwafrika wa kwanza kutunukiwa tuzo hiyo katika kipengele cha Fasihi. Katika maelezo kumhusu alielezewa kuwa ni mtu "ambaye katika mtazamo mpana wa kitamaduni na kwa sauti za kishairi ametengeneza drama ya kuwepo".

Wole Soyinka akipokea tuzo ya Nobel mwaka 1986. Picha kwa hisani ya Nairaland 

(ii) Tuzo ya Agip katika Fasihi kwa tawasifu yake ya Aké: The Years of Childhood.

(iii) Udaktari wa Heshima kwa kutambua mchango wake katika Fasihi na Harakati za utetezi Haki za Binadamu. Soyinka ametunukiwa Shahada hizo za Heshima na vyuo na vyuo vikuu zaidi ya 16 ikiwemo Havard, Oxford, Yale, Cambridge, Leeds, Cornell, Ibadan, Princeton, Obafemi Owolowo, Ibadan, École Normale Supérieure, Cape Town, Alberta, Neuchãtel, Toronto, Morehouse na vyuo vingine vingi. 

Wole Soyinka na wenzie walipotunukiwa Udaktari wa Heshima na Chuo Kikuu Cambridge mwaka 2022. Picha kwa hisani ya tovuti ya Cambridge

(iv) Commander of the Order of the Federal Republic (CFR) Hii ni miongoni mwa tuzo za hadhi ya juu aliyotunukiwa na serikali ya Naijeria. 

(v) Tuzo ya Academy of Achievement Golden Plate (2009)

(vi) Tuzo Maalumu (Special Prize) ya Kumbi za Michezo ya Maigizo ya Ulaya (European Theatre Prize) mwaka 2017. Alitunukiwa kwa "kuchangia katika utambuzi wa matukio ya kitamaduni ambayo yanakuza uelewa na kubadilishana maarifa kati ya watu"

(vii) Tuzo ya Anisfield-Wolf Books (1983) kwa tawasifu yake ya Aké: The Years of Childhood.

(viii) Mwanachama wa Jumuiya ya Kifalme ya Fasihi (the Royal Society of Literature) mwaka 1983.

(ix) Mwanachama katika Chama cha Lugha ya Kisasa (Fellow of the Modern Language Association)

(x) Alipewa Heshima ya kuwa Mwanachama wa Heshima katika jumuiya ya American Academy of Arts and Letters mwaka 1986.

(xi) Tuzo ya Kimataifa kuhusu masuala ya kibinadamu (International Humanist Award) na Umoja wa Kimataifa wa Kibinadamu na Maadili (International Humanist and Ethical Union) mwaka 2014.

(xii) Tuzo ya Desmond Tutu kwa Haki za Binadamu na Amani mwaka 2017.

(xiii) Tuzo ya Mafanikio katika Maisha (Lifetime Achievement Award) ya Anisfield-Wolf Book mwaka 2013.

(xiv) Medali ya The Benson aliyotunukiwa na Royal Society of Literature.

(xv) Tuzo ya Premi Internacional Catalunya mwaka 2007 ambayo alitunukiwa kwa kazi yake ya kukuza maarifa ya kitamaduni na kijamii.

(xvi) Tuzo ya Prince Claus mwaka 2008 ambayo alitunukiwa kwa kuthamini mafanikio yake kama mwandishi wa tamthilia.

(xvii) Medali ya William Edward Burghardt Du Bois ya Chuo Kikuu Harvard mwaka 2014.

(xviii) Tuzo ya Pak Kyong-ni mwaka 2017. Hii ni tuzo ya Kimataifa ya Fasihi iiliyoanzishwa Korea Kusini kama heshima ya kumuenzi maandishi wa riwaya wa Korea Kusini Pak Kyong-ni. Soyinka ni Mwafrika wa kwanza kutunukiwa tuzo hii.

(xix Mwanachama wa Heshima katika jumuiya ya Fasihi ya Naijeria (Literary Society of the Nigerian Academy of Letters)

(xx) National Order of Merit of the Federal Republic of Benin. 

 

MAISHA YA NDOA NA WATOTO

Soyinka amewahi kuoa mara 3 na katika ndoa zote alibahatika kupata watoto. Mwaka 1958 alimuoa Barbara Dixon huyu alikua mwandishi wa Uingereza. 

Mwaka 1963 alimuoa Olaide Idomu mkutubi huko Naijeria.

Mwaka 1989 alimuoa Folake Doherty ambaye ni mke wake mpaka sasa.

Soyinka ameyaweka mbali maisha yake binafsi kwa umma kwa hivyo hata taarifa zake binafsi nyingine wakati mwingine ni vigumu kuzifahamu. Jambo ambalo ameliweka wazi sana ni kazi zake kama mwandishi. 

Soyinka anao watoto 8 kutoka katika ndoa zote 3 alizowahi kufunga. Watoto wake wanaishi Naijeria na kufanya kazi katika kada tofauti tofauti.


KUFUNGWA GEREZANI NA MAISHA YA UHAMISHONI

Licha ya kuwa na wasifu mzuri katika taaluma ya fasihi duniani Soyinka amewahi kuwa na mgogoro na Serikali ya Naijeria. Mwaka 1967 alikamatwa kwa tuhuma za kuhusika na kuchochea vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Naijeria maarufu kama Biafra. Bila shaka unaikumbuka vita hii ambayo majimbo ya Kusini Mashariki mwa Naijeria yalijitangazia uhuru kamili na kutengeneza Jamhuri ya Biafra. Soyinka aliwekwa jela bila kutiwa hatiani kwa kosa lolote. Hii ilipelekea Soyinka kushikiliwa kama mfungwa wa kisiasa kwa miezi 27 (1967-1969) alipoachiliwa. Mwenyewe hukiri kwamba kipindi hiki cha ufungwa wa kisiasa kina mchango mkubwa katika uandishi wake na mtazamo kuhusu siasa na haki za binadamu.

Baada ya kuachiwa Soyinka alishiriki katika utengenezaji wa filamu aliyoiita Kongi ili kuhakikisha maudhui yanabaki kama alivyoandika. Filamu hii inatokana na kazi yake kwa jina Kongi's Harvest. Katika filamu hiyo Soyinka alitoa mtazamo wake kuhusu kupinga vikali utawala wa kijeshi nchini Naijeria.

Baada ya kutoka jela aliondoka Naijeria kwa kipindi kilichokadiriwa kuwa miaka 5. Katika miaka hiyo Soyinka alifanya kazi nchini Uingereza, Ufaransa na Ghana. Katika kipindi hicho Soyinka aliandika muswada wa tamthilia ya Jero's Metamorphosis (1973) ambayo ni muendelezo wa ile ya awali ya The Trials of Brother Jero. Humo kuna muunganiko wa ucheshi na kuonesha ukatili uliofanywa na utawala wa kijeshi kwa kutumia silaha dhidi ya watuhumiwa. Japokuwa Soyinka alituma nakala kwa waongozaji wa tamthilia nchini Naijeria hakuna aliyeonesha kuvutiwa na muswada wake kwa vile bado utawala wa kijeshi ulikua madarakani kwa hiyo waongozaji walihofia uhuru wao.

Mwaka 1994 aliondoka tena Naijeria kutokana na ukosoaji wake kwa Serikali ya kijeshi ya Jenerali Sani Abacha baada ya ule uhamishoni wa baada ya kutoka jela. Akiwa uhamishoni mara kwa mara alipaza sauti yake katika jumuiya za kimataifa kuingilia kati hali ya usalama nchini Naijeria hasa katika utawala wa Abacha. Alikosoa kuhusu rushwa, kukosekana kwa demokrasia na mauaji ya Ken Saro-Wiwa na washirika wenzie 8. Pia aliandika kitabu The Open Sore of a Continent (1996) ambacho kinazungumzia sana hali ya kisiasa barani Afrika hasa utawala wa kijeshi nchini Naijeria chini ya Jenerali Sani Abacha. Anakosoa na kuufananisha utawala wa kijeshi wa Jenerali Sani Abacha na kidonda kinachosababisha maumivu kwa taifa la Naijeria.

Picha kwa hisani ya Amazon

HARAKATI ZA HAKI ZA BINADAMU NA DEMOKRASIA 

Soyinka amekuwa mstari wa mbele katika harakati za haki za binadamu na demokrasia nchini Naijeria tangu enzi za ukoloni, kabla, wakati na baada kipindi cha kufungwa na kuishi uhamishoni.

Ameshiriki katika makundi mbalimbali ya kisiasa kama vile National Democratic Organization, National Liberty Council of Nigeria na PRONACO.

Alikua ni mkosoaji mkubwa wa utawala wa kijeshi wa Jenerali Sani Abacha (1993-1998) 

Pia, mwaka 2010 alianzisha chama cha Democratic Front for a People's Federation na akahudumu kama mwenyekiti.

Mwaka 2016, alisema kama Donald Trump angeshinda uchaguzi mkuu wa nchi ya Marekani basi angechana kibali chake cha kuishi katika nchi hiyo (American Green card) hii ni kwa sababu anasema hakuvutiwa na sera za Trump ambazo aliziona ni za kibaguzi na zinakinzana na haki za binadamu. Trump aliposhinda alitimiza ahadi yake hiyo japo si kwa kuchana kibali hicho bali alikifanya kisiweze kutumika. Ukosoaji wake kwa Trump na msimamo wake dhidi ya Marekani kwa wakati huo, sera na matamshi ya Rais yanaakisi wasiwasi wake mpana kuhusu siasa za kimataifa na haki za binadamu. Maoni ya Soyinka kuhusu Trump yanawiana na dhamira yake ya muda mrefu ya kuzungumza dhidi ya kile anachokiona kuwa dhuluma, ukandamizaji na ukosefu wa haki katika mazingira mbalimbali duniani.

Soyinka amekua mstari wa mbele kukosoa vitendo vyote vinavyokinzana na haki za binadamu ikiwemo udikteta. Ipo nukuu yake maarufu ambayo hutumiwa sana na wanaharakati wa haki za binadamu, demokrasia na ukosoaji, "The greatest threat to freedom is the absence of criticism" kwa tafsiri rahisi "jambo la kuogopesha kuhusu uhuru wa watu ni kukosekana kwa uhuru wa ukosoaji". Nukuu hii inalenga san ukosoaji wa masuala yote yanayofanywa na watawala na yanakinzana na utawala bora.


KWA UFUPI

• Alizaliwa Julai 13, 1934.

• Baba yake, Samwel Ayodele Soyinka alikua ni Mchungaji wa Kanisa la Anglikana na Mkuu wa Shule.

•Mama yake Grace Eniola Soyinka alikua na duka lakini pia alishiriki katika harakati za kumkomboa mwanamke nchini humo.

• Familia yake ni ya watu wa Yoruba, ambao utamaduni wao umeathiri kazi zake.

• Ni mwandishi mahiri aliye na kazi mbali mbali zinazohusu maigizo, mashairi na nathari (prose)

• Ukosoaji wake wa wazi dhidi ya tawala za kisiasa za Nigeria umechangia kuishi kwake nje ya nchi haswa Marekani ambako amewahi kuwa profesa katika vyuo vikuu mbalimbali.

• Shahada yake ya Awali alisoma Lugha ya Kiingereza katika Fasihi Chuo Kikuu cha Leeds.

• Mwaka 2005-2006 aliwahi kuwa kwenye Bodi ya Washauri wa Wahariri wa Encyclopaedia Britannica.

• Amewahi kufundisha katika Vyuo Vikuu vifuatavyo: Havard, Oxford, Emory, Loyola Marymount, Yale, Chuo Kikuu cha Nevada na vingine.

• Maandishi ya Soyinka yanachukua miongo mingi na yanajumuisha dhamira mbalimbali, kimsingi yanahusu mila za Kiafrika, udhalimu wa kisiasa na haki za binadamu.

• Amewahi kuigiza majukwaani nchini kwao Naijeria na Uingereza.


MENGINEYO

Maisha ya Soyinka yamebainishwa na dhamira yake isiyoyumba kwa haki za binadamu na uhuru wa kujieleza, na anasalia kuwa sauti yenye ushawishi katika fasihi na siasa.

Ingawa shughuli zake za kifasihi na kisiasa zimeandikwa vizuri, Soyinka ana mwelekeo wa kuweka maelezo ya maisha yake ya kibinafsi mbali na macho ya umma, kwa hivyo habari kuhusu ndoa na uhusiano wake hazijaangaziwa sana kwenye vyombo vya habari ukianganisha na zake za kikazi.

Soyinka ni mmoja wa waandishi wa Kiafrika waliopambwa zaidi na amepokea tuzo nyingi na sifa katika kazi zake zake za uandishi na uanaharakati.

Soyinka amekuwa na makongamano mengi ya kitaaluma na ya kifasihi yaliyoelekezw kumuenzi kwa kazi zake. Amekuwa akialikwa kama mzungumzaji mkuu katika hafla nyingi za kimataifa na kazi zake nyingi zimebadilishwa kuwa aina tofauti za kazi na hivyo kumfanya kuwa wa tofauti zaidi katika sanaa.

Kazi zake za kishairi mara nyingi hujikita katika mada za mila za Kiafrika, hali halisi ya baada ya ukoloni, msukosuko wa kisiasa, haki za binadamu, na makutano ya mapambano ya kibinafsi na ya kijamii.



MAKALA HII IMEANDALIWA NA KUANDIKWA NA VENANCE GILBERT KWA MSAADA WA VYANZO MBALIMBALI. WASILIANA NAMI KUPITIA

📞 0753400208

📧 venancegilbert@gmail.com

CELEBRITY: SHANIA TWAIN ANATIMIZA MIAKA 53 LEO AGOSTI 28, 2018

KUZALIWA 

Celebrity wetu wa leo ni Shania Twain. Jina lake la kuzaliwa ni Eilleen Regina Edwards lakini umaarufu wake umetokana na jina lilizoeleka la Shania Twain. Wengine wanamuita Malkia wa Muziki wa Country.  Alizaliwa mnamo Agosti 28, 1965 leo anatimiza miaka 53 ya kuwepo duniani. Alizaliwa huko Windsor, Ontario, Canada akiwa ni mmoja kati ya mabinti 3 wa Clarence na Sharon (Morison) Edwards. Yeye ndiye mkubwa. Alipokua na miaka 6 mama yake aliolewa tena na Jerry Twain ambaye alimchukua kama mwanaye. Alianza kuimba katika vilabu vya pombe na alipokua na miaka 13 alionekana katika The Tommy Hunter Show. Alipokua na umri wa miaka 22 wazazi wake waliuawa katika ajali na hivyo akaacha sanaa muziki ili awalee wadogo zake Mark na Darryl pamoja na dada zake wawili aliozaliwa nao kwa baba yake na mama yake mzazi. Mwaka 1991 alibadilisha jina lake alilopewa na wazazi wake na kujiita Shania Twain na hapo ndipo jina hili lilipokua.  Mwaka huo huo pia alisaini mkataba na lebo ya muziki ya Mercury Nashville.
Shania siku za hivi Karibuni.


KUOLEWA

Shania amewahi kufunga ndoa mbili ambapo ndoa ya kwanza alifunga na Robert John Lange Desemba 28, 1993 na ilidumu hadi Juni 9, 2010. Katika ndoa hii walifanikiwa kupata mtoto 1 kabla hawajaachana. Baadaye January 1, 2011 aliolewa na Frederic Nicolas Thiebaud ambaye yuko naye mpaka sasa. Hawajabahatika kupata mtoto. 

TUZO


Shania amewahi kushinda tuzo kadhaa na kutajwa katika nyingine:

Mwaka 1996 alitajwa katika tuzo za Grammy kama msanii bora chipukizi lakini hakufanikiwa kutwaa tuzo hiyo.


Mwaka 1997 aliteuliwa kuwania tuzo za Gemini katika kipengele cha mtumbuizaji bora katika vipindi mbalimbali vya television, huku pia hakufanikiwa kutwaa tuzo.

Mwaka 1998 aliteuliwa kuwania tuzo za MTV kama Video Bora ya Msanii wa Kike: You're Still the One. Huku pia hakufanikiwa kutwaa tuzo hiyo. Mwaka huu alishinda tuzo ya Grammy na wimbo wake wa From this Moment on.

Mwaka 1999 aliteuliwa kuwania tuzo ya Grammy kama Wimbo wa Mwaka: You're Still the One, pia hakufanikiwa kupata tuzo hiyo. 

Mwaka 2004 alifanikiwa kutwaa tuzo ya Bambi katika kipengele cha Pop Kimataifa. 

Mwaka 2005 Grammy walimchagua katika vipengele viwili; mtumbuizaji bora wa kike wa muziki wa country na kolabo bora ya country. Bado hakufanikiwa pia kutwaa tuzo. 

Mwaka 2011 alitwaa tuzo kama Nyota wa tuzo za Walk of Fame. 
Shania Twain katika video ya For evre and for always. 

ALBUM ZAKE

Shania Twain (1993)
The Woman In Me (1995)
Come Over (1998)
Up (2003)
Now (2017)

MENGINE KUHUSU SHANIA TWAIN

Anakula mboga za majani na alipendekezwa kua na mvuto kutokana na hili.

Mwaka 1995 aliorodheshwa kama Mtu mwenye majibu Halisi anapoulizwa maswali katika jarida la People Weekly.

Amewahi kukaa kwenye namba za juu za muziki duniani kwa wimbo wake You're Still the One ambayo ilishika namba 1 kwenye chati ya Billboard mara 7. Pia alishika namba 2 katika chati za Hot 100 kwa wimbo huo mwaka 1998.

Wimbo wake "Love Gets Me Everytime" ulikua ni wimbo ulioshika nafasi ya juu zaidi ya Billboard kwa wiki 5 katika nyimbo za country tangu wimbo wa mwisho wa Dolly Parton "Here You Come Again" uliposhika nafasi hiyo mwaka 1997.

Mwaka 1999 alitajwa kama mtumbuizaji bora wa muziki wa country na mwaka huo huo CMA walimtuza tuzo ya mwaka ya mafanikio katika muziki huo.

Mwaka 1999 aliuza nakala milioni 19 za albam yake ya Come Over nchini Marekani peke yake.

Mwaka 2003 aliwahi kushinda tuzo ya Juno ka Chaguo la Mashabiki.

Album yake ya Come Over (mauzo na matamasha) viliingiza dola za Marekani milioni 40 nchini Australia pekee. Hii inaifanya kuwa miongoni mwa album zilizowahi kushika chati za juu za muda wote nchini humo.

Alishika namba 39 katika orodha ya Jarida la Maxim kama mwanamke mwenye mvuto katika wanawake 100 waliotajwa katika orodha hiyo ya mwaka 2005.

Album yake ya Up (2002) iliuza nakala milioni 2 nchini Marekani ndani ya mwezi 1 tangu ilipowekwa sokoni.

Alipokua mdogo alikua na aibu na alikua Tom boy.

Amekua katika familia maskini ambayo chakula tu ilikua ni tabu. Shania alikua akienda shule bila kula kutokana na hali ya maisha kifedha nyumbani kwao.

Anapenda kushinda nyumbani na kupika. 
Anaamini kwamba yeye ni kama watu wengine.

Ni miongoni mwa wasanii wa 4 kutoka nchini Canada waliowahi kushika namba za juu katika chati ya Billboard tangu kuanzishwa kwake mwaka 1944. Wengine kutoka Canada ni Hank Snow, Anne Murray na Terry Klark.

Aliwahi kusema kwamba anapendezwa na majukumu wanayofanya wanaume katika maisha ya kila siku.

Shania anawasema kuwa anasikitika siku zote kwa kua ndoa yake ya awali alivunjika.

Anao wafuasi 863K katika mtandao wa Instagram. Katika mtandao wa Twitter anao wafuasi 901K. Katika mtandao wa Facebook anao wafuasi zaidi ya milioni 5. Ukurasa wake wa YouTube umetazamwa na watu bilioni 1.2 huku akiwa na subscribers zaidi ya bilioni 1.1.

Haya ni machache kati ya mengi niliyokuandalia kuhusu mwanamuziki Shania Twain. Kama una maoni usisite kuniandikia kupitia barua pepe: venancegilbert@gmail.com ama ujumbe Whatsapp 0712586027. Asante kwa kutembelea VENANCE BLOG na karibu tena kwa mengine mengi. 

RAIS MSTAAFU ALI HASSAN MWINYI ATIMIZA MIAKA 93: TUJIKUMBUSHE HISTORIA YAKE KWA UFUPI

Mei 8, 1925 wkati huo Tanganyika ikiwa ni koloni la Uingereza alizaliwa Rais mstaafu wa awamu ya pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mzee Ali Hassan Mwinyi.

Image result for MWINYI in marathon 

Alipoingia madarakani kumpokea aliyekuwa Rais wa Awamu ya kwanza,Mwalimu Julius Nyerere mnamo tarehe 5 Novemba mwaka 1985, watanzania wachache sana (kama wapo) waliweza kutabiri kwamba miaka kumi baadaye na zaidi baada ya kustaafu rasmi, ataibuka kuwa mmojawapo wa maraisi wa Tanzania ambao watabakia kupendwa na kuheshimika kwa namna ya kipekee kabisa. Tunadiriki kusema “namna ya kipekee” kwa sababu ukweli unabakia kwamba inapofanyika tathmini ya uongozi wake, bado mtu au watu mbalimbali wanakuwa na maoni yao tofauti tofauti kuhusiana na suala hilo. Utoaji huo wa tathmini ni suala ambalo haliwezi kukoma leo wala kesho, ni tukio linaloendea na litakaloendelea, vizazi mpaka vizazi. Huo ndio uzuri au ubaya wa historia na muda (history and time) huwa vina jinsi ya kipekee katika kutoa hukumu zao.

Mpaka anakabidhi madaraka yake ya Urais kwa Rais wa awamu ya tatu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa mnamo tarehe 23 November mwaka 1995, jina ambalo wengi tulipenda kulitumia ni “Mzee Ruksa” ingawa kamwe hatukuwahi kusahau kwamba jina lake kamili ni Ali Hassan Mwinyi, Raisi wa awamu ya pili wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Ali Hassan Mwinyi alizaliwa tarehe 8 mwezi wa tano (Mei) mwaka 1923 katika kijiji cha Kivure,wilayani Kisarawe, mkoa wa Pwani,Tanzania Bara. Kama wengi wa viongozi wetu, Mwinyi naye alizaliwa katika iliyokuwa Tanganyika. Akiwa bado mwenye umri mdogo sana familia yake ilihamia Zanzibar. Kwa maana hiyo Mwinyi ni mzaliwa wa bara aliyekulia na kuendelea kuishi visiwani Zanzibar.

Alianza safari yake kielimu huko visiwani Zanzibar katika shule ya msingi Mangapwani kuanzia mwaka 1933 hadi 1936 kabla ya kujiunga na shule ya sekondari Dole kwa ajili ya elimu ya sekondari kuanzia mwaka 1937 mpaka mwaka 1942. Baada ya hapo alijiunga na Chuo Cha Ualimu Zanzibar kusomea ualimu kuanzia mwaka 1943 mpaka 1944.
Mwinyi katika picha rasmi ya wakati wa utawala wake.

Kuanzia mwaka 1945 mpaka mwaka 1950 alirejea tena katika shule ya Mangapwani,shule aliyosomea,safari hii akiwa sio mwanafunzi tena bali Mwalimu.Kuanzia mwaka 1950 mpaka 1954 alikuwa Mwalimu Mkuu wa shule hiyo wakati huo huo alikuwa akiongeza elimu yake kwa njia ya posta ambapo alijipatia General Certificate in Education (GCE) na pia alikuwa amejiunga na Durban University Institute of Education, United Kingdom (kwa njia ya posta tena) kusomea stashahada ya ualimu. Baada ya hapo alijiunga tena na Chuo Cha Ualimu Zanzibar kama mkufunzi kuanzia mwaka 1956 mpaka mwaka 1961 huku pia akiendelea kujisomea kwa njia ya posta kutoka Regent Institute kilichopo London nchini Uingereza ambapo alijipatia cheti cha ufundishaji lugha ya kiingereza.

Kuanzia mwaka 1961 mpaka 1962 alijiunga na Hall University, Uingereza katika Tutors’ Attachment Course. Mzee Mwinyi pia ana cheti ya lugha ya kiarabu alichokipatia Cairo nchini Misri kati ya mwaka 1972 na 1974.

Safari yake ya kisiasa aliianza rasmi mwaka 1964 alipojiunga na Afro Shiraz Party (ASP) huko Zanzibar ambapo alikitumikia chama katika ngazi na nafasi mbalimbali. Kati ya mwaka 1964 na 1965 alikuwa ni Katibu Mkuu wa muda katika wizara ya elimu Zanzibar kabla hajateuliwa kuwa Naibu Mkurugenzi katika iliyokuwa Zanzibar State Trading Corporation (ZSTC).Hiyo ilikuwa ni kati ya mwaka 1965 na mwaka 1970. Pia katika miaka hiyo hiyo,kuanzia mwaka 1966 mpaka 1970, Mwinyi alikuwa mweka hazina msaidizi katika tawi la ASP la Makadara,Zanzibar. Wakati huo huo pia kati ya mwaka 1964 mpaka 1977 alikuwa ni mwenyekiti wa Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA)
Majukumu mengine aliyokuwa nayo miaka hiyo ni pamoja na uenyekiti wa Zanzibar Censorship Board (1964-1965), Mjumbe wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dar-es-salaam na pia mwenyekiti wa Baraza la Chakula na Lishe.

Mwinyi (kushoto) akiwa na maraisi wenzake wastaafu Benjamini Mkapa (kulia) na Jakaya Mrisho Kikwete (katikati)

Kuanzia mwaka 1972 mpaka 1975, Mwinyi alikuwa ni Waziri wa Afya wa Tanzania kabla ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani kuanzia 1975 mpaka 1977. Mwaka 1977 aliteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Misri cheo alichokitumikia mpaka mwaka 1982 aliporejea nyumbani na kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii cheo ambacho alikutumia kwa muda mfupi tu kwani mwaka 1983 aliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi katika ofisi ya Makamu wa Raisi.
Mwaka 1984, kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Raisi wa Zanzibar wakati huo,Alhaj Aboud Jumbe, Mwinyi alichaguliwa kuwa Raisi wa Zanzibar, Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar na wakati huo huo Makamu wa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuanzia mwezi August mwaka huo huo wa 1984 Mwinyi alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi cheo alichoendelea nacho mpaka mwaka 1990 baada ya kung’atuka kwa Hayati Mwalimu Nyerere kutoka katika kukiongoza Chama Cha Mapinduzi(CCM)

Mwinyi (wa pili kutoka kushoto) akishuhudia mchezo wa bao kati ya hayati Mwalimu Nyerere (wa pili kutoka kulia) na mzee mmoja wa Butiama(jina halijulikani).Wengine wanaoshuhudia ni Mama Maria Nyerere(kulia) na kaka yake Nyerere,Chief Burito(wa tatu kutoka kulia).Picha ilipigwa Butiama.

Lakini kabla ya hapo, mwaka 1985,Mwinyi alichaguliwa kuwa Raisi wa Awamu ya Pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia kustaafu kwa Mwalimu Nyerere. Mwinyi ni mtaalamu wa lugha ya Kiswahili na pia hupenda michezo hususani jogging. Mwinyi ameoa wake wawili (Sitti Mwinyi na Khadija Mwinyi), ana watoto na wajukuu. Anaishi Msasani jijini Dar-es-salaam.

Related image
Rai mstaafu Mwinyi akiwa na wastaafu wenziye Mkapa, Kikwete na Rais Magufuli. Picha kwa hisani ya Mwananchi Communication Limited.
MAKALA HII NI HAKIMILIKI YA JEFF MSANGI MWANDISHI WA TOVUTI YA BONGOCELEBRITY.

MOHAMMED SALAH: ILIKUAJE AKAIMARIKA HARAKA? MAJIBU HAYA HAPA

Mohammed Salah
Huku wachezaji wakisherehekea kwa fujo baada 4-0 dhidi ya ENPPI, kocha Said Al Shesheni aliangalia upande mmoja na kugundua kwamba mchezaji mmoja wa kikosi cha al-Mokawloon wa kikosi cha wachezaji wasiozidi umri wa miaka 16 hakuwa akifurahia michuano iliokuwa Cairo. Alikuwa akibubujikwa na machozi kwamba jina lake halikuwa katika orodha ya wafungaji mabao. Akicheza kama beki wa kushoto ilikuwa vigumu kuchukua jukumu kubwa kama alivyotaka.
Akiwa mzaliwa wa eneo la Nagrig, kijiji kimoja kilichopo kilomita 130 Kaskazini mwa mji mkuu wa Misri, mchezaji huyo alilazimika kupitia tatizo la kusafiri kwa saa tisa kila siku mara nyingine akilazimika kutumia mabasi 10, ili kuweza kufika mazoezini mbali na kushiriki mechi.
Na baada ya kufurahishwa na ari ya kijana huyo Al Sheheni alimpatia fursa na kumpeleka safu ya mbele. Tangu wakati huo Mohammed Salah hajarudi nyuma tena.
Kijana katika uwanja wa Mo salah
Mchezaji huyo wa Liverpool alilazimika kulipia uwanja mpya katika shule yake ya zamani.

Habari hiyo ni jibu kwa swali ambalo limekuwa katika fikra za mashabiki wa soka duniani: Mchezaji ambaye hakuwa na athari yoyote kimchezo katika ligi kuu za Ulaya mara moja amekuwa mfungaji bora akilinganishwa na Lionel Messi na Christiano Ronaldo.
Katika soka inasaidia wakati mchezaji anapojikuta katika eneo analohitajika kuwa na katika wakati ufaao. Lakini ni watu wachache waliokuwa na hilo wakati Liverpool ilipotangaza usajili wa Salah kutoka klabu ya Italia ya Rome mwaka uliopita .
Kitita cha $55.7m kinaonekana kuwa cha juu kwa mchezaji ambaye alikuwa amefeli kuonyesha umahiri wake katika soka ya Uingereza baada ya kuhudumu kwa zaidi ya mwaka mmoja akiwa Chelsea 2015.
Pia ni muhimu kuona kwamba Misri sio timu yenye umaarufu mkubwa katika soka duniani, ijapokuwa ina umaarufu mkubwa barani Afrika, baada ya kushinda taji la kombe la Afrika mara saba.
Lakini The Pharaoh wamecheza katika michuano miwili ya kombe la dunia 1934 na 1990 na hadi Salah alipoimarika, ilikuwa rahisi kutajwa kwa kuwa kipa Essam El-Hadary yuko katika harakati za kuwa mchezaji mkongwe zaidi kushirki katika kombe la dunia, wakati Misri iliporejea katika kinyang'anyiro hicho nchini Urusi.
Timu ya taifa ya Misri
Misri imeshiriki katika michuano miwili pekee ya kombe la dunia lakini wamefaulu kushiriki Urusi 2018

Ni nini kilichofanyika kimakosa kwa Salah mapema alipocheza Uingereza? Kwanza Salah alishiriki katika ligi ya Switzerland, ambayo haina ushindani mkubwa kama ile ya Uingereza.
Akiwa Chelsea pia alikabiliwa na ushindani mkubwa kutoka kwa wachezaji walioimarika na hakupata fursa za kutosha kuonyesha umahiri wake.
Raia huyo wa Misri alicheza mechi 19 kwa klabu hiyo ya London huku akianzishwa katika mechi tisa pekee. Ni mara mbili pekee alipocheza dakika zote 90. Salah baadaye alipelekwa kwa mkopo kwa vilabu vya Italia kabla ya kusainiwa na Roma kwa msimu wa 2015/16
Ni wakati huo ambapo Salah alionyesha umahiri wake na kufunga mabao 34 katika misimu miwili kabla ya kuelekea Liverpool.
Image result for mohamed salah with mourinho at chelsea
Salah hakuweza kufanya vizuri chini ya usimamizi wa Mourinho akiwa Chelsea: Alicheza mechi 19 na kufunga mabao 2 pekee.
"Alikuwa mtoto alipowasili Chelsea na Chelsea ilikuwa na kikosi kizuri hivyo basi ilikuwa vigumu'', alisema mkufunzi wa Liverpool Jurgen Klopp akizungumza na runinga ya Ujerumani wiki hii.
"Nadhani sote lazima tukubaliane kwamba Jose Mourinho ni kocha mzuri kwa hivyo mara nyengine mambo huwa hivyo. Kwa hivyo iwapo haiwezekani jiondoe ujaribu tena na hivyo ndivyo ilivyokuwa na Mohamed."
Katika ziara ya hivi karibuni Anfield, Mourinho, ambaye sasa ni mkufunzi wa Manchester United alionekana akimkumbatia raia huyo wa Misri.
Na mahojiano na ESPN Brasil yaliorushwa hewani Jumapili iliopita, raia huyo wa Ureno alizungumza kwa mara ya kwanza kuhusu uhusiano wake na mchezaji huyo.
''Ni mimi ndiye niliyemsaini Salah na uamuzi wa kumuuza haukuwa wangu, bali ulikuwa wa Chelsea''.
''Ni mtu mzuri , lakini alikuwa mdogo na hakuwa amejiandaa kimaungo na kifikra wakati alipwasili. Pia alipata utamaduni tofauti. Nafurahi sana kumuona anaendelea vyema, hususan kwa sababu hajafunga dhidi ya United'', alifanya mzaha.
Image result for mohamed salah with klopp
Kocha wa Liverpool Jurgen Klopp akimkumbatia Mohammed Salah
Inawezekana kwamba magoli aliyofunga katika msimu wa 2017/18 yalipita kiwango ambacho mchezaji huyo alikuwa ametaka kuafikia. Katika mechi 48 alizochezea Liverpool katika mashindano yote, raia huyo wa Misri alifunga mabao 43 na kusaidia pasi za mabao 15.
Amekuwa nyota katika kombe la vilabu bingwa Ulaya ambapo ameisaidia Liverpool kukaribia kufika fainali ya kombe hilo kwa mara ya kwanza tangu 2007.
Raia huyo wa Misri ni baraka kwa aina ya mchezo wa Klopp kwa kasi na mashambulio.
Mbali na mafanikio yake, Salah anaweza kufanikiwa kuwa mchezaji wa kwanza wa Afrika kushinda taji la mfungaji bora Ulaya, taji analokabidhiwa mfungaji bora katika ligi ya Ulaya.
Na msimu wa Salah hautakamilika katika wikendi ya mwisho ya ligi kuu ya Uingerza. Timu ya taifa imefanikiwa kufuzu katika kombe la dunia la 2018 ikiwa ni mara kwanza katika kipindi cha miaka 28 baada ya kampeni ya kuwania kufuzu ambapo Salah alifunga mabao matano kati ya manane huku akitoa usaidizi wa mabao mawili.
Ushujaa wake ulihusisha penalti ya dakika 94 dhidi ya Congo ambayo ilikamilisha kufuzu kwa taifa hilo katika kombe la dunia .
Mo Salah akiichezea Egypt
Salah alifunga mabao matano kati ya magoli ya Misri katika kombe la kombe la dunia.
Na kudhania kwamba kuimarika kwake kulianza kwa bahati. Mnamo mwezi Machi 2012, soka la Misri lilikuwa limedorora: ligi ya taifa hilo ilisitishwa kutokana na janga la uwanja wa Port Said - maandamano ambayo mapema takriban watu 70 walifariki huku wengine 500 wakijeruhiwa.
Huku wakitafuta kushiriki katika mechi kwa maandalizi ya michezo ya Olimpiki mjini London, timu hiyo ya Misri yenye wachezaji wasiozidi umri ya miaka 23 walipanga mechi za kirafiki hidi ya vilabu vya Ulaya.
Mojawapo ni klabu ya Uswizi ya Basel, ambaye rais wake, Bernhard Heusler, alimsajili Salah hapo kwa hapo.
"Kulikuwa na baridi kali lakini alionyesha mchezo mzuri. Alicheza kipindi cha pili pekee lakini sijaona mchezaji mwenye kasi katika maisha yangu yote'', alisema Heusler.
Wachezaji wenza wa Basel wanakumbuka kwamba Salah hakuchezshwa mara moja. Katika mwaka wake wa kwanza katika klabu hiyo mchezaji huyo alitumiwa kama mchezaji wa ziada na ni katika mechi 10 pekee kati ya 29 ambapo alicheza kwa zaidi ya saa moja.
Mchezaji mwenza Philipp Degen, aliambia Sky Sports habari kuhusu Salah alivyomshangaza kila mtu baada ya kufunga bao la ushindi dhidi ya Chelsea katika mechi ya kombe la vilabu bingwa.
Salah akiichezea Basel
Salah alijiunga na Basel mwaka 2012 baada ya kucheza kipindi kimoja pekee ya mechi dhidi ya timu ya Usiwzi
"Tulijaribu kumpa hongera lakini hakukubali. Anasema kuwa alipiga nje mikwaju sita na ni wa saba tu pekee kwa kuwa klabu ilimuamini. Umaruufu wake pia unatokana na kuwa mfuasi mkuu wa dini ya Kiislamu.
Anapendwa sana nchini Misri wakati ambapo taifa hilo limegawanyika katika misingi ya kisiasa ilioanzishwa mika michache iliopita na maandamano ya Uarabuni na mapinduzi ya 2013, lakini Salah anapenda mizizi yake.



Amelipia ujenzi wa shule na hospitali na kuweka jina lake katika mashirika ya hisani ikiwemo kuchangisha $280,000 kwa hazina ya serikali inayolenga kuimarisha kiuchumi familia za Wamisri masikini.
Picha ya Mo Salah mjini Cairo
Mchezaji huyo ni shujaa wa taifa lake la Misri.
Utata unaozunguka jina la Salah unashirikisha madai kwamba alikataa kusalimiana na wachezaji kutoka klabu ya Israel ya Maccabi Tel-Aviv katika mechi dhidi ya Basel mwaka 2013 - alienda kubadili viatu vyake kabla ya mechi kuanza wakati huo raia wengi wa Misri walikuwa wamepinga vitendo vyake na hata kumtaka mchezaji huyo kutoshirikishwa katika mechi ya ugenini ya Israel.
Hata hivyo mbali na kuzomewa na mashabiki wa Maccabi Salah alicheza mechi ya ugenini na kufanikiwa kufunga bao.
Wiki iliopita baada ya raia huyo wa Misri kuisaidia Liverpool kushinda 5-2 dhidi ya Roma katika kombe la vilabu bingwa, Waziri wa Ulinzi Avigdor Lieberman alituma ujumbe katika mtandao wa Twitter kwamba atampigia mkuu wa utumishi wa umma kumsaini Mohammed Salah kwa mkataba wa kudumu na jeshi la Israel.

Chanzo: BBC
Picha: Getty Images