VIFAA VYA KUWATAMBUA WENYE UGONJWA WA EBOLA VYAINGIZWA NCHINI

Serikali imeanza kuingiza nchini vifaa vya kuwabaini watu wanaohisiwa kuwa na dalili za ugonjwa wa homa kali ya ebola ambavyo vitawekwa kwenye viwanja vya ndege pamoja na baadhi ya maeneo ya mipakani. Jana Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Steven Kebwe alikabidhi mashine nne za kuwapima abiria wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege bila kuwagusa. Vifaa hivyo vinabaini mtu kuwa na dalili za ebola kutokana na joto lake na abiria wanapimwa kwa kumulikwa machoni na kwenye masikio. Kwa kuanzia mashine hizo ambazo ni mfano wa kamera zitapelekwa kwenye viwanja vya ndege vya Mwanza, Kilimanjaro, Zanzibar na Dar es Salaam. Maeneo hayo kwa mujibu wa naibu waziri huyo ndiyo yanapokea wagonjwa wengi kutoka nje ya nchi. Dk Kebwe pia aliagiza shehena ya mashine zingine zitakazoingizwa nchini kuanzia leo zipelekwe kwenye viwanja vingine vya Mtwara, Kigoma na maeneo ya mipakani kuhakikisha kuwa kila abiria anayetoka nje ya nchi anapimwa dalili za ugonjwa huo hatari. Pia aliagiza wanadiplomasia na viongozi wa kitaifa wanaotoka nje ya nchi ambako wanakwenda kuhudhuria mikutano mbalimbali pia wapimwe kwani ugonjwa hauchagui cheo wala fedha na hadhi aliyo nayo mtu. Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifwani alisema jana kuwa wamenunua mashine hizo nne kutoka Afrika Kusini, lakini zimetengenezwa nchini Marekani kwa kiasi cha Sh milioni 16. Alisema katika kipindi hiki ambacho kuna mlipuko wa ugonjwa wa ebola huko Afrika Magharibi, upatikanaji wa vifaa hivyo ni adimu na haiwezekani kupata mashine zote kwa msambazaji mmoja, hivyo akasema leo ziwawasili mashine nyingine mbili kutoka Ubelgiji. Mkurugenzi wa Manunuzi wa MSD, Heri Mchunga alisema mashine hizo kitaalamu zinajulikana kama thermo scanners ni mashine za mkononi na kila abiria atakayeshuka uwanja wa ndege atapimwa kwenye macho au masikio bila kugusana.

Comments

Popular Posts

ZIFAHAMU NCHI ZINAZOZUNGUMZA KISWAHILI BARANI AFRIKA

HISTORIA YA KOMBE LA DUNIA TANGU 1930, WAANDAAJI & WASHINDI

WALIOCHAGULIWA CHUO CHA MIPANGO MAJINA HAYA HAPA

CELEBRITY: SHANIA TWAIN ANATIMIZA MIAKA 53 LEO AGOSTI 28, 2018

MKUTAO WA G7 KUANGAZIA USALAMA NA MAZINGIRA

WAFAHAMU MATAJIRI 10 WA TANZANIA MWAKA 2018

FAHAMU MAMBO HAYA 20 KUHUSU TANZANIA

KANSELA ANGELA MERKEL ASEMA UJERUMANI YA SASA NI BORA ZAIDI